
Salim Said Salim Mwandishi wa habari mkongwe Zanzibar
MWISHONI mwa wiki sehemu ya nyuma ya jengo maarufu na la kihistoria
la Beit el Ajaib (Nyumba ya Ajabu) liliopo Forodhani, Mjini Unguja,
liliporomoka. Kwa bahati njema hayakutokea maafa makubwa, lakini
kuanguka kwa majumba haya katika sehemu mbalimbali za Mji Mkongwe ni
hasara kubwa kwa historia ya mji wa Zanzibar.
Tukio hili la kuporomoka kwa jengo la Beit el Ajaib, lililopo
pembezoni mwa Ngome Kongwe iliyojengwa na watawala wa Kireno, ni
kuendelea kuporomoka majengo ya zamani, baadhi yao yalijengwa takribani
miaka 200 iliyopita katika Mji Mkongwe.
Jengo hili la ghorofa tatu, kila moja likiwa na urefu wa zaidi ya
futi 40 ambalo linatazama na bandari ya Zanzibar, lilijengwa na Sultan
Seyyid Barghash bin Said (1880-88), ni la ina yake na hakuna
linalofanana nalo katika Afrika ya Mashariki.
Kwa muda mrefu sasa jengo hili maarufu duniani kote, kama yalivyo
mengine mengi ya zamani ya Mji Mkongwe wa Zanzibar, yameonekana kuchakaa
na kuhitaji matengenezo ya haraka.
Baadhi yamekuwa yakiporomoka moja baada ya jingine, hasa wakati wa
mvua za masika au vuli na hata kusababisha maafa na hasara kubwa.
Kwa kweli hali iliyojitokeza ni ya kusikitisha. Hata hivyo, baadhi ya
majumba haya, yamefanyiwa ukarabati mkubwa kwa misaada kutoka taasisi
za Umoja wa Mataifa na nyingine za kimataifa. Miongoni mwao ni iliyokuwa
nyumba ya sultani, zahanati ya jamii ya Ismalia na nyingine nyingi.
Majengo yaliyofanyiwa ukarabati sasa yanapendeza na kuwa vivutio kwa
watalii, lakini toka kufanyiwa ukarabati huo zaidi ya miaka 15
iliyopita, hakuna juhudi za kuyatunza na labda yanangojewa yachakae na
kutafutiwa misaada ya kuyakarabati kutoka nje.
Majumba haya ya zamani na njia nyembamba za sehemu ambazo yapo, ndiyo
yaliyosababisha Mji Mkongwe wa Zanzibar kuvutia utalii na kutangazwa
kama urithi wa dunia.
Lakini jambo la kusikitisha ni kuona yametupwa na serikali. Wakati
umefika kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na wananchi wa Visiwani kwa
jumla kutambua kuwa Mji Mkongwe ni urithi unaotaka kuenziwa na
kutoruhusu kupotea.
Sio vibaya kutarajia nchi za nje na mashirika ya kimataifa kusaidia
kutunza majengo haya ya kihistoria, lakini ni aibu na fedheha kuona wao
ndio wanaotarajiwa kuyashughulikia.
Hii ni historia ya Zanzibar na ni watu wake ndio wanaowajibika kwanza kuyatunza na wageni kusaidia tu.
Kwa muda mrefu sasa nchi yetu imebweteka kwa kutegemea misaada hata
ya kutengeneza bustani au ujenzi wa vyoo vya shule. Tumejenga utamaduni
wa kuona hiyo ni kazi ya wageni na sio yetu, kama vile historia ya
Zanzibar haina uhusiano na watu wake.
Lazima kwa serikali na wananchi kubadilika na kuyaona majengo haya ya
kale, hasa yale yenye historia ya kuvutia kama Beit el Ajaib,
yanatunzwa na kushughulikiwa ipasavyo.
Kichekesho kingine ni kwamba panapotokea taasisi ya Visiwani kutafuta
fedha za kukarabati majengo ya zamani, kama lilivyofanya Baraza la
Biashara, wamiliki wa viwanda na wakulima kwa jumba maarufu la mvumbuzi
wa kiingereza, David Livingstone, baadhi ya viongozi wa serikali huja
juu kutaka majengo haya yakabidhiwe serikali.
Hivyo serikali ilikuwa wapi wakati majengo haya yalipokuwa karibu
kuporomoka? Huu sio mwenendo mzuri hata kidogo na unawakatisha tamaa
Wazanzibari wanaoipenda nchi yao na wenye nia njema ya kusaidia
kuyatunza majengo haya ya zamani.
Mwenendo huu hauna maelezo yoyote yale isipokuwa ni kielelezo cha roho mbovu kwa baadhi ya watu waliopo madarakani.
Tuache tabia hii inayowavunja moyo wananchi kwani kuyakakarabati na
kuyatumia majengo hayo haina maana kwamba wameyataifisha kwani yanabakia
kuwa mali ya serikali na wao kama wananchi ni sehemu ya serikali.
Kwa sasa tunapaswa kubadilika na kuwa na mpango maalumu wa kutenga
vifungu vya fedha katika bajeti zetu za matumizi ya serikali ya kila
mwaka kwa ajili ya kuyahudumia majengo haya ya kihistoria tuliyorithi
kutoka kwa wazazi wetu.
Tukumbuke kuwa watalii wengi na wana-historia hufika Zanzibar
kuyaangalia majengo haya ya kihistoria, lakini tukiyaruhusu kuporomoka
hao watalii watakuja Zanzibar kufanya nini?
Wakati umefika na kwa kweli tumechelewa, kwa serikali kuhakikisha
kuwa katika bajeti yake ya matumizi ya kila mwaka panatengwa fungu
maalumu la kuyashughulikia majengo ya zamani, hasa yale ya kihistoria.
Kama tunaweza kutafuta fedha kujenga majumba mapya ya wizara za
serikali na kuonekana kuwepo mashindano ya kufanya hivyo, kwanini
tushindwe kutafuta fedha za kuilinda historia yetu? Ni kweli haiwezekani
kuyakakarabi yote kwa wakati mmoja, lakini inawezekana kuifanya kazi
hii kwa uwamu.
Kinachohitajika ni kuwepo mpango mzuri badala ya sehemu kubwa ya
mapato ya serikali kutumika kwa safari za viongozi zisokwisha na
kujinunulia magari ya fahari kwa viongozi na watumishi wa idara na
taasisi za serikali.
Haya yanafanyika huku tukijigamba kwamba ati tunafanya kila juhudi za
kupunguza umasikini unaowakabili watu wetu. Huku ni kujidanganya na
wananchi wanajiuliza masuala mengi na kukosa majibu.
Sio vizuri kujikita kwa mambo ya fahari na anasa na kuipa mgongo
historia yetu. Vizazi vijavyo havitatusamehe kama tutayatelekeza majengo
haya na kupotea na watu kubaki kuhadithia habari za majengo haya wakati
yakiwa yameshatoweka. Hawatatusamehe hata kidogo kwa kushindwa
kuwarithisha historia hii tuliorithi kutoka kwa wazazi waliotutangulia
mbele ya haki.
Watajiuliza hawa wazee wetu walikuwa watu wa aina gani na wakati huo hatutakuwepo katika dunia hii kujitetea.
Tuchukuwe juhudi sasa ya kuhifadhi maeneo muhimu ya historia Unguja
na Pemba ili historia isije kutuumbua kwa kuipoteza sehemu muhimu ya
historia ya Zanzibar na watu wake.