Sunday, December 9, 2012

Shambulio la guruneti Eastleigh laua 5


Idadi ya vifo kutokana na shambulio la guruneti karibu na msikitii huko kitongoji cha Eastleigh cha Kenya iliongezeka na kufikia watu watano siku ya Jumamosi (tarehe 8 Disemba) baada ya wahanga watatu kufariki kutokana na majeraha wakiwa hospitalini, shirika la habari la AFP liliripoti.
Siku ya Ijumaa, guruneti lilirushwa katika kundi la watu wakati waumini walipokuwa wanaondoka toka msikiti maarufu wa Hidaya.
"Tumewapeleka maafisa zaidi kwenye eneo la tukio ili kuhakikisha kuwa kuna amani," Mkuu wa Polisi wa Nairobi Moses Nyakwama alisema.
Watu 16 zaidi wako hospitalini wakipatiwa matibabu, polisi na maafisa wa hospitali walisema. Mbunge wa Kamukunji Yusuf Hassan na mlinzi wake walilazwa katika hospitali ya Aga Khan mjini Nairobi, na wengine wako katika Hospitali ya Taifa ya Kenyatta.
Tukio hilo linafuatia mlipuko wa bomu la kando ya barabara ambalo liliuwa mtu mmoja huko Eastleigh siku ya Jumatano.
Kiasi cha washukiwa 90 wametiwa mbaroni kuhusiana na mashambulizi hayo mawili, alisema Katibu Mkuu wa Wizara ya Usalama wa Ndani Mutea Iringo.
"Baadhi ya washukiwa waliokamatwa ni wakimbizi ambao walitoroka kutoka kambi za wakimbizi," alisema, kwa mujibu wa Capital FM ya Kenya. "Tutaendesha operesheni nchi nzima ili kuhakikisha kuwa wakimbizi wanarejeshwa Dadaab."
Iringo, akifuatana na Kamishna wa Mkoa Njoroge Waweru, aliwataka Wakenya kuisaidia polisi katika juhudi zao za kuwakamata waliohusika na mashambulizi hayo

Vikosi vya Somalia na AMISOM vyadhibiti Jowhar


Jesho la Taifa la Somalia (SNA), likisaidiwa na wanajeshi kutoka Misheni ya Umoja wa Afrika nchini Somalia (AMISOM), vilichukua udhibiti wa Jowhar kutoka kwa wanamgambo wa al-Shabaab mwishoni mwa wiki, Shirika la Habari la Taifa la Somalia liliripoti siku ya Jumapili (tarehe 9 Disemba).
Vikosi hivyo vya washirika viliuteka uwanja wa ndege na maeneo ya karibu ya Burane na Mahaday kabla ya kuuteka mji, ambao ni mji mkuu wa jimbo la Shabelle ya Kati. Bila ya kuendelea na vita, wanamgambo wa al-Shabaab waliukimbia mji na kuelekea kusikojulikana, shirika hilo la habari liliripoti.
SNA na AMISOM sasa wana udhibiti kamili wa Jowhar, alisema mkuu wa SNA Jenerali Abdikarin Yussuf Dego-badan, kwa mujibu wa Redio Bar-Kulan inayofadhiliwa na Umoja wa Mataifa.
Jowhar ni makazi ya pili kwa ukubwa katika Shabelle ya Kati kutekwa kutoka kwa kikundi cha wanamgambo wa al-Shabaab mwaka huu, kufuatia kukombolewa kwa Balad mwezi wa Juni.