Saturday, August 3, 2013

Rais mpya wa Iran ashika madaraka


Rais mteule wa Iran Hassan Rouhani anaapishwa katika sherehe mjini Tehran ambapo atapewa idhini ya kiongozi wa kidini nchini humo, Ayatollah Ali Khamenei.
Hassan Rouhani
Rouhani ambaye alikuwa mpatanishi kwenye mazungumzo ya mradi wa nuklia wa Iran, alishinda uchaguzi wa urais nchini Iran katika duru ya kwanza.
Wakati wa kampeni zake rais huyo mteule aliahidi kuleta mabadiliko ya kijamii na kiuchumi, na alisema ataimarisha uhusiano kati ya taifa hilo na jamii ya kimataifa ambao uliharibika zaidi wakati wa utawala wa Rais Mahmoud Ahmedinejad.

Nambari ya dharura 999 yarejea Kenya


Nambari hiyo haijatumika kwa zaidi ya miaka 15
Polisi nchini Kenya wameambia BBC kuwa nambari ya kupiga wakati wa dharura 999 imeanza tena kutumika baada ya miaka 15 ingawa watu wanapiga simu za utani.
Mwezi Julai mahakama iliamua kuwa polisi werejeshe huduma hiyo mwishoni mwa mwezi Julai, lakini BBC ilipojaribu kupiga simu hiyo haijibiwi kamwe.
Polisi walilazimika kufunga huduma hiyo mwaka 1998, kwa kutokuwa na uwezo wa kukabiliana na mahitaji ya wananchi.
Wenyeji walilazimika kupiga nambari za simu ambazo zilikuwa ndefu sana kuweza kupata huduma za polisi wakati wa dhahrura.
Ilikuwa bora kwa wenyeji kwenda kwa kituo cha polisi kupata huduma walizohitaji au kuripoti kisa cha uhalifu kuliko kupiga simu kutaka kusaidiwa na polisi.
Mkuu wa polisi mjini Nairobi Benson Kibui aliambia BBC kuwa tangu nambari hii kuanza kutumika tena , watu wamekuwa wakipiga simu za utani wakijidai kutafuta hoteli.
Pia kulikuwa na idadi kubwa ya watu waliokuwa wanajaribu kuona ikiwa inafanya kazi.
Mwanaharakati wa Kenya Okiyo Omtatah alikwenda mahakamani akitaka nambari hiyo kuanza kutumika tena .